pesayetu
Hali ya Miundomsingi Kaunti ya Isiolo
June 2023
PesaYetu
article

Share

Kwa miaka mingi, kaunti ya Isiolo imeshuhudia hali duni ya miundomsingi kama barabara. Hapo awali, hali hii ilichangia wakaazi kuandamana kama njia moja ya kushurutisha serikali kukarabati barabara mbovu.  

Kulingana na ripoti ya CDIP, kaunti ya Isiolo iko na mtandao wa barabara wa kilomita 1275.5. Kati ya hii, kilomita 42 ni za lami. 

Kama njia moja ya kuwekeza sekta ya uchukuzi, kaunti ilikadiria kutenga fedha za ujenzi wa barabara za mjini na vijijini. Ripoti ya CDIP inaonyesha kuwa serikali ya kaunti ilipanga kutenga shilingi milioni 559 kwa kipindi cha miaka tano kwa mradi huu. 

Licha ya kuwa na mtandao mkubwa wa barabara, swala nyeti ni ikiwa wakazi wananufaika ipasavyo? Barabara hizi huharibika kunaponyesha kwa sababu ya matope.

Baadhi ya maeneo yaliyoathirika sana ni Korbesa na Kinna amabapo changamoto ya barabra mbovu huwathiri haswa akina mama wajawazito na wagonjwa kufika katika vituo vya afya.

Kwengineko, wakaazi wa eneo la Mabatini,  wadi ya Bula Pesa wamelalamikia barabara mbovu ambayo imesababisha usafiri kuwa ngumu.

Kwa upande wake Ali Muhammed ambaye ni mkazi wa eneo la Kambi Shariff, alielezea hali mbaya ya barabara imefanya shughuli nyingi kulemazwa hususan kunaponyesha.

Licha ya changamoto hizo, uzinduzi wa kilometa 744 ya barabara ya Isiolo – Mandera – Wajir inaonekana kuwa ya kuleta matumaini makubwa kwa wakaazi wa Gambela na Modogashe kwani itafungua nafasi nyingi za kazi miongoni mwa vijana , anavyosema bwana Jillo Guyo ambaye ni mkaazi.

Kulingana na Guyo, eneo hilo limeshuhudia kiwango cha chini kibiashara lakini sasa anaona nuru. 

Kwa mujibu wa ripoti ya bajeti ya mwaka 2021/2022 kaunti ya Isiolo ilitenga mamilioni ya fedha kuboresha miundo msingi katika wadi zifuatazo ;

Wabera ilipokea mgao wa shilingi milioni 20 kujenga barabara za cabros ambapo mradi huo unaendelea. Bulapesa ilitengewa milioni 20, Burat milioni 15, Ngaremara milioni 12, Kinna milioni 13, Garbatulla milioni 15, Sericho milioni 13, Cherab milioni 15.

Mwaka jana, gavana alizindua mpanga wa kukarabati barabara kaunti ya Isiolo baada ya malalamishi miongoni mwa wakazi. 

Licha ya fedha hizo kutengwa na serikali ya kaunti kuendeleza mradi wa kujenga barabara katika maeneo hayo , bado hali imesalia ilivyo na kuzidi kuongeza changamoto kwa wakaazi ambao hutegemea barabara kuendesha shughuli zao za kila leo.

Image: A road in Isiolo county. Source: KID

Makala Haya Yamechapishwa na Baliti Fm Kwa Ushirikiano Na Code For Africa, Kenya Community Media Network Na Baraza La Vyombo Vya Habari Katoliki (Cameco) Kupitia Msaada Kutoka Ushirikiano Wa Ujerumani Kama Sehemu Ya Mradi Wa Jukumu Letu La Kaunti Yetu.

logo
This site is a project of Code for Africa, the continent’s largest network of civic technology and data journalism labs. All content is released under a Creative Commons attribution Licence 4.0. Reuse it to help empower your own community.

2022 PesaYetu

Stay in touch with us
instagramfacebooktwitterlinkedin